Friday, May 25, 2012

Hatuyapendi maisha haya, jamii inatuonea!

Na Fredy Azzah

NI wazi kuwa chini ya jua hakuna mtu au binadamu yeyote anayependa kudhalilishwa, kila mtu angependa kufanya kazi halali ili awe na uhakika na kipato chake.Hivyo basi, ukilitambua hilo utakuwa na sababu ya kutumia jicho la tatu na kutafakari mambo mbalimbali yanayotokea katika jamii.Baadhi ya watu ambao pengine jamii imekuwa ikiwaangalia kwa jicho ambalo nadiriki kusema siyo sahihi, ni wasichana pamoja na wanawake ambao huuza miili yao katika maeneo mbalimbali nchini.Watu wengi wamekuwa wakiwatupiwa lawama kutokana na shughuli hiyo wanayofanya,  kila siku wakipewa majina mbalimbali kama vile machangudoa, dada poa, malaya na mengine mengi.Wakati jamii ikilitazama hivyo kundi hili, kwa upande wao nao wanailaumu  jamii kuwa ndiyo iliyowafikisha hapo walipo.Hivi karibuni  katika mazungumzo na baadhi ya  wanawake hao wanaofanya shughuli hiyo katika maeneo mbalimbali ya Dar es Salaam, wengi wao wanasema kutelekezwa na familia zao ama waume zao, ndiyo sababu kubwa iliyowafikisha wengi wao hapo walipo.




Winfrida Rafael (49), ni mmoja kati ya watu hao mwenye umri mkubwa na pengine mkongwe katika biashara hiyo kutokana na kuifanya kwa takribani miaka 15 sasa tangu alipotelekezwa na mume wake.
“Nilikuwa ninaishi Mwanza na mume wangu wakati huo alikuwa anafanya kazi katika benki moja, baadaye alifukuzwa kazi, tukahamia Dar es Salaam na mwaka 1997 ndiyo alinikimbia kabisa na kuniacha na mtoto mchanga yeye akakimbilia Mtwara,” anaeleza mama huyo.

Anafafanua kuwa, kutokana na ugumu wa maisha ndipo alipolazimika kuingia kwenye biashara hiyo ili aweze kujikimu kimaisha.

Tangu mama huyo aanze kufanya biashara hiyo, mwaka 2002 alijigundua pia kuwa na maambukizi ya virusi vya Ukimwi (VVU) ambayo hata hivyo anasema hajui aliambukizwa kwa njia gani.

“Siwezi kujua kama huu ugonjwa nimeambukizwa na wanaume ama ni katika kuuguza ndugu zangu kwa sababu nimewauguza ndugu zangu wengi mpaka wakafariki na wakati ule kulikuwa hakuna elimu sana ya kutosha kuhusu ugonjwa huu kwa hiyo kujikinga ilikuwa ni vigumu,” anasema Winifrida.

Anaeleza pia kuwa, pamoja na kuwa na ugonjwa huo pamoja na kansa ya mguu aliyoipata baada ya ajali aliyopata mwaka 2005, analazimika kuendelea kufanya biashara hiyo ili aweze kupata walau chakula cha kuishi.

Ni kutokana na hali hiyo anasema kuwa, afya yake imekuwa ikizorota kwa kasi ambapo CD4 zake zimekuwa zikishuka  na kuwa  kati ya 200 na 300 badala ya kuwa 600  hadi 1,000 kama zinavyohitajika katika mwili.

Anasema kuwa ingawa anajua hali hiyo inasababishwa na kufanya ngono ambazo wakati mwingine anafanya zisizo salama, hana njia nyingine ya kuweza kumsaidia kuishi.

Naye Diamonte Mandanda (29), yeye anasema amejikuta akiingia kwenye biashara hiyo miaka miwili iliyopita baada ya kutelekezwa na mwanaume ambaye ni raia wa Italia aliyezaa naye.

Anasema tayari  baba yake na mama yake walishafariki na kuwa yeye alikuwa akiishi kwa mama yake mkubwa ambaye hata hivyo baadaye walishindana na kuamua kusaka mahali pa kuishi na kujitegemea.

Akiwa anaishipeke yake na  kujiendeleza na shughuli ndogondogo, anasema alimpata mwanaume huyo wa Kiitaliano ambaye walipenda sana na baadaye kwenda kuishi nchini Kenya ambako baadaye familia ya mwanaume huyo ilimkataa na hivyo kurudi nchini (Tanzania) na mwanae.

Hata baada ya kurudi nchini, Diamonte anasema baba wa mtoto amekuwa hataki kutoa matumizi yoyote kwa ajili ya kumsaidia mwanaye hali anayosema inamlazimu kufanya shughuli hiyo ili kutafuta riziki yake na mtoto.

Anasema kuwa, licha ya kuushirikisha ubalozi wa nchi hiyo (Italia) juu ya suala hilo, mpaka sasa wameshindwa kumsaidia na anaendelea kuishi maisha ya taabu yeye na mwanaye.

“Jamani mimi nawaasa wasichana wenzangu tusiwe na tabia za kuwapapatikia wanaume wa Kizungu, kuna wasichana wengi sana wameachiwa watoto na tunawalea sisi wenyewe na kibaya zaidi huko mitaani watoto wetu wananyanyapaliwa kweli,” anasema na kuongeza:

“Hata ukienda dukani kutaka kununua kitu wanakucheka wanakuambia kamwambie Mzungu akununulie, mpaka najiuliza kwani watoto wetu siyo binadamu, kwa nini watu watunyanyapae,” anahoji dada huyo kwa uchungu.

Anasema kuwa, kwa mtu atakayeweza kumsaidia akaachana na biashara hiyo, atakuwa amemsaidia kwa kiasi kikubwa kwani anachokitamani katika maisha yake ni mtoto wake huyo kupata haki zake za msingi kutoka kwa mzazi mwenzie.

Kwa upande wake, Josephine Rutta (26), anasema kuwa wazazi wake wapo kijijini Mkoani Kagera na kwa kiasi kikubwa wanamtegemea yeye na sasa mtoto mdogo na mzazi mwenzake hamsaidii kwa chochote.

Baadhi ya watu wanaojishughulisha na kundi hili lililosahaulika ni taasisi ya Dhahabu Arts.

Katibu Mkuu wa taasisi hiyo, Hussein Wamaywa anasema taasisi yake imeliona tatizo hilo na imeamua kulifanyia kazi.

Anasema kuwa, ili kupunguza kasi ya maambukizi ya Ukimwi kwa wasichana hao, wameamua kuwapa elimu ya jinsi ya kujikinga dhidi ya  virusi vya Ukimwi pamoja na kuwapa njia mbadala ya kuachana kabisa na biashara hiyo.

Anasema kuwa, shughuli hiyo inafanikishwa kwa ushirikiano na  Rapid Fund Envelope (RFE), ambao wametoa fedha kwa ajili ya kuwapa wasichana hao mafunzo pamoja na mikopo ili wafanye shughuli nyingine na kuachana na biashara hiyo.

 “Kutokana na hali hiyo, tumeona kuwa njia pekee ya kupambana na hali hii ni kutoa elimu juu ya Ukimwi, kinga na maambukizi pamoja na elimu ya ujasiriamali lengo likiwa ni kuhakikisha tunawatoa kabisa katika janga hili,” anasema Wamaywa.

Anasema kuwa, walengwa watatoka katika kata 90 za Dar es Saalam ikiwa ni kata 30 kwa kila manispaa na kwamba zaidi ya wasichana na wanawake 3,600 watafikiwa.

“Kwa wateja wao kwa sababu hatuwezi kuwafikia moja kwa moja, tutatumia matangazo ya redio kufikisha ujumbe,” anasema Wamaywa.

Anasema kuwa, tayari wameshafanya mafunzo kwa wasichana wanaofanya biashara hiyo katika wilaya zote tatu za jiji la Dar es Salaam, Ilala, Kinondoni na Temeke.

“Sasa kazi tuliyowapa ni kutengeneza vikundi na kubuni miradi ambayo sisi tutawafadhili, tunataka wawasaidie pia na wenzao kwa kuwapa elimu juu ya maambukizi ya ukimwi na ile ya ujasiriamali,” anasema.

Mwisho
Machangudoa:hatuyapendi haya, jamii inatuonea www.faceboo.com

No comments:

Post a Comment