Thursday, May 24, 2012


Mila za Kimasai zinavyobariki ubakaji



Fredy Azzah

Katika Wilaya ya Sumajiro, suala la ubakaji wazawa wa eneo hili ambao kwa kiasi kikubwa ni wamasai na waarusha, wanasema lipo kwa kiasi kidogo na kwamba linaletwa sana na wahamiaji katika eneo hili.
Hata hivyo kauli za wazawa wa eneo hili zinakinzana na zile za baadhi ya watendaji wa serikali na wananchi wasiyo katika eneo hili wanaosema ubakaji ni mkubwa.
Hata hivyo vitendo vya ubakaji vinaonekana kutoripotiwa kwa wingi katika polisi, ingawa vinaelezwa kutendeka.
Kwa mujibu wa taarifa za Wilaya ya Sumanjiro, kwa mwezi kunaripotiwa matukio kati ya matatu mpaka matano.
Wengi wanaoeleza kuwepo kwa matukio hayo kwa wingi, wanasema yanafanyika sana katika ngoma ya kimasai inayoitwa Esoto.

“Ukiniambia nieleze ukubwa wa tatizo la ubakaji katika jamii ya Simanjiro nitakuambia ni karibu asilimia 90 ya watoto wanabakwa,” anasema Mtendaji wa Kata ya Endonyongijape Mary Chisoji.


Anasema kuwa, kwa kiasi kikubwa matukio haya yanafanyika katika ngoma hizo ambazo vijana maarufu kama morani, hufanya ngono na watoto wa chini ya miaka 10 ambao wengi wao wako darsa la tatu au la nne, hali anayosema inasababisha watoto wengi kupata mimba na kuacha shule.

“Kwenye hizo ngoma utakuta hivi vitoto vimevaa vizuri sana kuliko wenzao, wamejipanga msitari na morani wamejipanga wakiwa wanaimba, morani anaenda na kumgusa msichana na rungu,” anasema na kuongeza:

“Kama msichana aliyeguswa na morani ametolewa mahari tayari, utamkuta na yeye anaenda anatoa kichwa kwa morani alafu anarudi, ngoma hiyo huchezwa usiku kucha na katika hiyo hali ndiyo ubakaji utokea sana.”

 Anasema kuwa, anaamini ni kutokana na ngoma katika shule ya msingi Orkirungrung kumekuwa kuna matukio mengi ya mimba na wasicha kuacha shule ambapo mwaka jana matukio 4 ya mimba katika eneo hilo yaliripotiwa.



Kwa upande wa polisi, wanasema kwa kiasi kikubwa matukio ya ubakaji hayaripoti polisi na mara ningi hata yale machache yanayoripotiwa yanakuja kukosa ushahidi.



Mrakibu wa Polisi Wilaya ya Simanjiro (ASP) Felix Kikwala, akizungumza kwa niaba ya Kamanda wa Polisi wa Wilaya hiyo, anasema hali hiyo inachangiwa na jamii hiyo kuwa na tabia ya kuficha siri hata kama jambo limamuumiza.

“Watu wa huku ni wasiri sana, matukio mengi ya ubakaji yanayoripotiwa ni yale tu ya maeneo ya mijini lakini huko vijijini sana hawaripoti, wengi wanamalizana hukohuko,” anasema na kuongeza:

“Lakini hata kwa wale wanaoripoti mara nyingi wanakuja wamechelewa na kutafuta ushahidi inashindikana, mtu anabakwa leo anakuja kutoa taarifa kituo cha polisi baada ya mwezi mmoja, ama mwingine anaoga ama kama ni mtoto amebakwa anamuogesha, akija huku sisi tunashindwa kutafuta ushahidi.”

lakini pamoja na mambo hayo, madiwani wanasema katika maeneo yao hakuna matukio ya ubakaji.

“Katika kata yangu sijawahi kusika mambo ya ubakaji kabisa,” anaeleza Diwani wa Langai Jackson Lesikari ambaye anaungwa mkono na Diwani wa Orkasument Naftali Samuel.

Madiwani hawa wanaeleza hivyo wakati katika kituo cha polisi Sumanjiro takwimu zinaonyesha kwa kipindi cha mwezi kesi tatu za ubakaji ziliripotiwa.

Kwa upande wake Mganga Mkuu wa Kituo cha Afya Orkesument Loishorua Ole Yamat, anasema mara chace sana wamekuwa wakipata matukio ya ubakaji ambapo kwa mwaka jana walipata mawili na mwaka juzi moja.

Hata hivyo anasema kuwa kwa kiasi kikubwa waathirika wa matukio hayo hufika hospitali wakiwa wamechelewa, hivyo kushindwa kupata ushaidi kama kweli wamebakwa ama vipi.

“Kuna mwingine anakuja akiwa ana karibu mimba ya kujifungua ndiyo anasema amebakwa, sasa katika hali hiyo tunakuwa hatuna cha kumsaidia zaidi ya kupima tu kama ana maambukizi ama vipi,” anasema Mganga Mkuu Msaidizi Ester Mshange.

Anasema wengi, hukaa karibu mwezi baada ya kubakw baada ya hapo ndipo huenda hospitali.

“Kinachochangia mara nyingi ni umbali kutoka huko vijijini,” anasema Dk Mshange.

Huku Dk Ole Yamati, akisema kuchelewa huko husababishwa na tabia ya wamasai kuficha siri, “Katika mila za kimasai kuja kumwishitaki mtu ni kosa, mara nyingi wanakaa huko na kuelewa wayamalize kinyumbani, wakishindwa ndiyo huja hospitali huku tayari wakiwa wamechelewa,”

Kauli ambayo inaungwa mkono pia na ASP Kikwala, anayesema mara wamasaidi mtu akifanya kosa huwa na taratibu za kutozana faini huku adhabu kubwa ikiwa ni kutoa dume la ng’ombe ambalo huchinywa na kuliwa.

“Ukienda kuishitaki, unaweza mpaka kutengwa ama kupewa laana, wanaamini hivyo wao,” anasema.

Wakuu hao wa hospitali hiyo, hata hivyo wanasema kwa upande wao wana dawa za PEP,  abazo hutakiwa kupewa mtu aliyebakwa ndani ya saa 72 baada ya tukio kutokea ili aweze kukingwa na magonjwa ya zinaa ikiwemo ukimwi.

Huku ASP Kikwala akisema kuwa, tabia ya wamasai kuhamahama kutafuta malisho ya mifugo, kwa kiasi kikubwa hukwamisha kesi mbalimbali kutokana na kukosena ili watoe ushahidi juu ya suala fulani pale inapohitajika.

Baadhi ya wananchi akiwemo Martha Okida (50) mkazi wa kijiji cha Njiro anaeleza kuwa, ubakaji katika eneo hili ulianza kuonekana baada ya eneo hili kuwa na mwingiliano wa makabilia.

“Watu wa makabila walipoanza kuja hapa ndiyo tulianza kusikia sehemu fulani kabakwa mtoto na mambo mengine kama hayo, matukio kama haya kwa mwaka unaweza kuyasikia mara moja ama hata usisikie kabisa,” anasema Okida.

Kauli ya Okida inaungwa mkono na Jacobo Lemburis mkazi wa kata ya Langai kijiji cha Narokusaito, anayesema ubakaji katika eneo hili haupo kabisa.

“Mimi ni mkazi wa eneo hili nimezaliwa huku lakini vitendo vya ubakaji sijawahi kuvisikia huku,” anasema

Kwa uapande wa Ofisa Maendeleo ya Jamii katika eneo hilo Kaanaeli Kaaya, anasema kwa hajawahi kupata suala lolote linalohusiana na ubakaji wa aina yoyote katika eneo hilo.

“Ila siyo kuwa hakuna kabisa vitendo vya ubakaji, lakini ukubwa wa Wilaya ya Simanjiro ambayo ni sawa kabisa na nchi za Rwanda na Burundi, inaweza ikawa ndiyo sababu ya hizi taarifa kutofika katika ofisi zetu,” anasema Kaaya.

Kaaya hatofautiani sana na Hakimu wa Mahakama ya Mwanzo Simanjiro Steve Mibagayo, anayesema hajawahi kupokea kesi ya ubakaji katika Mahakama hiyo.

Pia naye Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya hiyo Patrick Saduka, anasema vitendo vya ubakaji katika eneo hilo hajawahi kuvisikia ingawa anasema serikali ya Wilaya hiyo pamoja na mashirika machache yasiyo ya kiserikali wamekuwa wakitoa elimu juu ya kuheshimu utu pamoja na haki za wanawake na watoto.

No comments:

Post a Comment