Uozeshaji
wanafunzi, watoto wachanga unavyoshamiri Simanjiro
mmoja wa wanafunzi aliyefanikiwa kuendelea na masomo ya sekondari baada ya wenzake watatua lofaulu nao kuolewa wote.
Fredy Azzah
“SISI ukiwa na mtoto wa kike tayari unahesabu
utajiri, sasa ni mtu gani mjinga utakubali kufa na njaa umwache mtoto akamalize
miaka saba shuleni,” anasema Elibariki Kisongo mkazi wa Kirun’gurun’gu.
Mzee huyu wa makamu ya miaka 70, anasema kuwa
licha ya kuwa na wasichana 13 aliozaa na wake zake watano hakuna hata mmoja
aliyesoma.
“We acha ujinga bwana, nikiwasomesha alafu
watakuja kunisaidia nini,” anasema mzee huyo anayesema huwaoza watoto wake
wakioneka wakubwa ingawa anashindwa kujua huwa wanakuwa na miaka mingapi.
Kwa upande wake Martha Okida (50), mkazi wa Orkesument, anasema ili mtoto wa kike asome katika jamii
ya kimasai, mzazi wake anahitajika awe na akili ya ziada.
“Siku hizi baada ya kujua kuwa kumuolewa kwa
mtoto wa shule ni vibaya, wanawapeleka kwa mume wakiwa na miaka sita mpaka
nane,” anasema mama huyo.
Anasema kuwa, kuna matukio mawili ya watoto
wenye miaka nane walikuwa wameozwa kwa wazee wenye zaidi ya miaka 65, ambao
hata hivyo waliwahi kuokolewa na watu wa Sirika lisilokuwa la Kiserikali la Nafgem
na kwenda kuwasomesha mjini Moshi mkoani Kilimanjaro.
Anasema pia kuwa, kwa wale walio shuleni
wakitaka kuolewa hupewa mimba ili wafukuzwe shuke ama wazazi wao kuwaambia
wafanye vibaya shuleni.
“Mimi ili mtoto wangu asiole, ilibidi niende
shuleni niongee na walimu waje kuwachukua, lakini nikamwambia mwalimu nyumbani
nitamkana ili baba asinipige, baba alipokuja na kutaka kunilaani akaambiwa nilienda
shuleni nikafukuzwa Mungu akasaidia watoto wangu wakasoma,” anasema mama huyo.
Kauli ya mama huyo inaungwa mkono na Elibariki
Morani anayesema hali ya kuwaozesha watoto wadogo walio chini ya miaka 10,
yameshika kasi katika eneo hilo.
“Hawa watoto siyo kuwa wanaenda moja kwa moja
kwa mume, kwakuwa utakuta tayari mzee amechukua mahari, basi inabidi wampeleke
mtoto akalelewe na mama wa kijana aliyetoa mahari, akiwa mkubwa aanze kuishi
naye kama mke,” anasema kijana huyo.
Hata hivyo, suala linalozua mjadala hapa ambalo
hata kauli za watoa taarifa hazikufafanua, ni jinsi ya kutambua kwamba mtoto
amekuwa na anaweza kuishi na mume.
Wakati morani akisema ni mtoto kutoka mazima,
Jacobo Lemburis anasema kuwa, wakinamama ambao wanawalea watoto hawa
wakijiridhisha kuwa mtoto anaweza kulala na mwanaume bila kujali ana miaka
mingapi, basi anaruhusiwa kufanya hivyo.
“Kwa hiyo huku kwetu wanaoachishwa masomo ili
waolewe ni wachache kwa sababu wengi hawapati hata hiyo nafasi ya kuingia
darasa la kwanza,” anasema Lemburisi.
Lemburis pamoja na Martha, wanasema kuwa, moja
ya sababu inayochangia hali hii ni wazazi kuwa na tamaa ya kupata mahari.
“Wanajua kabisa kuwa ni kosa kuozesha watoto
lakini wanatamaa ya mali,” anasema Lemburisi.
Hata hivyo kwa upande wake Martha, anasema kuwa,
kwa kiasi kikubwa wanasiasa wamekuwa hawakemei ipasavyo vitendo hivyo kwa kuhofia,
kupoteza nafasi walizo nazo.
Mrakibu wa Polisi Simanjiro (ASP) Felix Kikwale,
anasema matukio haya yanaripotiwa kwa kiasi kidogo sana polisi kwani tangu
mwaka huu uanze ni tukio moja tu limeripotiwa.
“Siyo kwamba haya matukio hayapo, tunajua ni
mengi sana lakini watu hawaripoti polisi kwa kutojua sharia ama kwa tabia zao
tu za usiri na kuogopa laana,” anasema Kikwale.
Mwenyekiti wa kijiji cha Lalumorijoi Jeremia
Lemandi, anasema katika kata yake hivyo vitendo hivyo hakuna kabisa.
Pia Diwani wa kata ya Langai, Jackson Lesikari
anasema kuwa, suala hilo lipo kwa kiasi kidogo ingawa anasema hana takwimu huku
akisema suala hilo linasababishwa na watu kutokuwa na elimu.
“Wazazi wengi hawajui kuwa kumuozesha mtoto wa
chini ya miaka 18 ni kosa, lakini kuna mashirika na serikali yamekuwa yakitoa
elimu,” anasema Diwani huyo.
Naye Diwani wa Orkesument Naftal Samuel anaunga
mkono kauli hiyo akisema kuwa, “Wananchi wangu wengi wameelimika, siyo rahisi
ukute wakiozesha watoto.”
Mkuu wa Shule ya Sekondari Orkesument Jacobo
Khahima inayohudumia wanafunzi kutoka
kata za Orukasument, Endonyongijape na Langai, anasema hana ushahidi wa kutosha
juu ya suala hilo, ingawa kuna baadhi ya wanafunzi wamekuwa wakiacha shule na
wengine kupata ujauzito, jambo analosema linaweza kuhusishwa na hali hiyo.
“Hatuwezi kusema kuwa wanaolewa moja kwa moja,
lakini wapo ambao wanaacha shule na wengine mimba, yote haya yanaweza
kuambatana na suala la kuolewa,” anasema Mwalimu
Anasema kuwa, tangu Januari mpaka sasa tayari
wamepata wanafunzi wawili wajawazito mmoja aliyetakiwa kuwa kidato cha tatu
sasa na mwingine wa kidato cha kwanza.
“Huyu wa kidato cha kwanza yeye alikuja na mimba
kutoka huko kwenye shule yake ya msingi,” anasema Khahima.
Pia anasema kuwa, mpaka sasa wanafunzi sita wa
kidato cha kwanza hawajaripoti shuleni hapo licha ya kupangiwa na Serikali na
kuwa, mara nyingi watoto wengi wamekuwa wakienda likizo na kutorudi shuleni.
Joyce Michael mwanafunzi wa kidato cha nne
katika shule hiyo, anasema kuwa wanafunzi wengi wamekuwa wakipewa mimba na matokeo
yake kuacha shule.
“Wapo wengi tunaosoma nao wakiwa wameshaolewa,
wakirudi likizo wanaenda kuishi kwa waume zao na wakipata mimba wanaacha shule,
lakini mara nyingi hawa huwa hawaoni maana ya kusoma kwa sababu wanajua tayari
wanawaume.” Anasema Michael.
Naye Naomi Meshilieki mwanafunzi wa kidato cha
nne katika shule hiyo anasema kuwa, katika kata ya Nangai anapotoka, suala la
wanafunzi kuachishwa shule na kuolewa siyo jambo la ajabu.
“Tulipomaliza shule tulikuwa sita ambao
tulifaulu, wenzangu wawili waliolewa na wengine waliacha shule wenyewe na sasa
ni kama watatu tu tumeendelea,” anasema Meshilieki.
Mtendaji wa Kata ya Endonyongijabe Mary Chisoji
anasema kuwa, suala la watoto kuachishwa shule katika kata yake ni kubwa.
Anasema tatizo hilo katika kata yake yenye shule
moja tu ambayo ni ya msingi ya
Orkirungrung ni kubwa, jambo ambalo limechangia hata matokeo ya shule hiyo kuwa
mabaya.
“Mwaka jana katika shule hii watoto wote
walifeli, ilibidi tukutane wadau wa elimu kuangalia tatizo ni nini, moja ya yaliyogunduliwa
ni wazazi kuwaeleza watoto wao wafanye vibaya ili waolewe ama wakachunge
Ng’ombe,” anasema Chisoji.
“Hili tuliambiwa na badhi ya wanafunzi, na
wamasai kwasababu wanaamini kuwa mzazi anaweza hata kukulaani ukikataa
walichokwambia, nao kweli wakafanya vibaya, kwa hiyo hili suala la watoto wa
kuachishwa shule lipo tena kwa sura nyingi tu.”
Kauli hiyo inaungwa mkono pia na Ofisa Elimu
Msingi wa Wilaya hiyo Jackison Mbise, anayesema kuwa, kuachishwa shule huko
huja kwa sura mbalimbali.
Anasema kuwa, moja ya njia hizo ni pamoja na
wanafunzi kubeba mimba kwa makusudi ili wafukuzwe shule na nyingine ni utoro.
“Unaweza kukuta kati ya wanafunzi 194 wanaoanza
shule, wanakuja kumaliza kati ya 40, 70 ama 100, wengine wanatoweka kwa njia
kama hizi, wengi wa hawa wanaocha shule ni wasichana, ingawa na wanaume kwa
uchache wapo na wao huenda kuchunga Ng’ombe”
Anasema kuwa, njia nyingine ni mzazi kuhama
kabisa katika Kijiji kwa kisingizo cha kwenda kutafutia mifugo malisho, lakini
ukweli ni kuwa wanaenda kuwaozesha watoto.
Katika Shule za sekondari hali ni mbaya zaidi
katika eneo hilo la wanafunzi kuachishwa shule, hali inayofanya Ofisa Elimu
Sekondari katika Wilaya hiyo Julius Mduma, kusema kila kukicha wanaumiza kichwa
kuangalia jinsi ya kuangalia tatizo hilo.
Anasema kuwa, katika Wilaya hiyo yenye Shule za
Sekondari 14, kati ya Wanafunzi 1976 wasichana wakiwa 934 na wavulana 1,042
waliopangwa kujiunga na kidato cha kwanza mwaka huu, walioripoti shuleni mpaka
Aprili 16 mwaka huu walimuwa 1283 wasichana wakiwa 606 na wavulana 677.
“Kwa hiyo mpaka sasa Wanafunzi 491 wasichana
kati yao wakiwa 272 na wavulana 219 hawajafika shuleni, Wilaya tumekuwa tukitoa
gari kila mara likawatafute huko vijini bila mafanikio,” anasema Ofisa huyo.
Mbali na hao ambao walikwepa kuanza kidato cha
kwanza, anasema pia hata wale ambao hufanikiwa kuanza kidato cha kwanza, zaidi ya nusu huwa hawahitimu kidato cha
nne.
Takwimu za Wilaya hiyo zinaonyesha kuwa, kati ya
wanafunzi 157 walionza kidato cha kwanza mwaka 2004 wavulana wakiwa 70 na
wasichana 87, waliohitimu kidato cha nne mwaka 2007 ni 47, wavulana wakiwa 30
na wasichana 17.
Pia mwaka 2005 walianza kidato cha kwanza
wanafunzi 334, wavulana wakiwa 185 na wasichana 149, na waliohitimu kidato cha
nne mwaka 2008 ni 154, wavulana wakiwa 94 na wasichana 60.
Mwaka 2006, wanafunzi 400 wavulana wakiwa 200 na
wasichana 200 walianza kidato cha kwanza, waliohitimu mwaka 2009 walikuwa 350,
wavulana wakiwa 195 na wasichana 155.
Mwaka 2007, wanafunzi 754 walianza kidato cha
kwaza wavulana wakiwa 361 wasichana 393, walioitimu mwaka 2010 walikuwa 622
wavulana wakiwa 340 na wasichana 282.
Kwa mwaka 2008 Takwimu za Wilaya hiyo pia
zinaonyesha kuwa, wanafunzi walioanza kidato cha kwanza waliwa 1,431 wavulana
wakiwa 720 na wasichana 711, waliohitimu kidato cha nne mwaka 2011 walikuwa 763
wasichana wakiwa 363 na wasichana 363.
“Hilo ndiyo tatizo kubwa la huku, na kwa kweli ukiangalia wasicha wengi
wanaoacha shule tatizo ni mimba na kuolewa,” anasema Ofisa Huyo.
Uchunguzi uliofanywa na Mwananchi kwa Kushirikiana
na Tamwa, umebaini kuwa sababu kubwa inayochangia mimba kwa wanafunzi kuwa
nyingi katika eneo hili, ni Ngoma maarufu kama Esoto ambazo huchezwa usiku
kucha na morani pamoja na wasichana ambapo wenyeji wanasema baada ya ngoma
wanaume na wasichana hufanya ngono kwa kile kinachoitwa ni kuwafundisha
wasichana hao ambao ni wachumba wao.
Mtendaji wa Kata ya Endonyongijape Mary Chisoji,
anasema hilo ni jambo ambalo amewahi kulishuhudia na kuwa ni tatizo kubwa sana
kata yake.
Anasema kuwa, baada ya kuchezwa ngoma hizo ambazo
wasicha wanaoshiriki huwa wameshakeketwa na wapo tayari kwa kuolewa, hufanya
ngono na Morani kwani tayari kimila wanatambulika kama ni wachumba na tayari
huwa wamesha lipiwa mahari.
Morani Saitoti (38), mkazi wa Orkujit anakiri kuwepo kwa ngoma hizo na kusenma
kweli vitendo hivyo vinafanyika, lakini yeye anasema haoni tatizo kwani tayari
wasicha ambao hucheza ngoma hizo ni wachumba wa watu.
“Sasa kuna ubaya gani kama utatoka na msichana
wako ambaye umeshamtolea mali,” anahoji Saoitoti.
Pia katika eneo hilo, wasicha kuolewa wakiwa
bado wakiwa ni wanafunzi ni tatizo kubwa.
Hakimu wa Mahakama ya Mwanzo Simanjiro Steve
Mibeyazo, anasema kuwa kesi za watoto kuachishwa shule zimekuwa zikifikishwa
katika mahakama hiyo na maofisa watendaji wa kata na zimekuwa zikitolewa uamuzi.
Hata hivyo anasema sheria iliyopo sasa ina
changamoto kwa kuwa, haisemi msichana
aliyepata mimba anatakiwa achukuliwe hatua gani na kuwa, amekuwa akitumia uzoefu wake katika kutoa
adhabu kwa wote.
No comments:
Post a Comment